Dunia
Dunia (kutoka neno la Kiarabu; wakati mwingine pia: ardhi na kwa neno asili la Kibantu nchi) ni gimba la angani ambapo juu yake tunaishi sisi binadamu na viumbehai wengine wengi, tukipata mahitaji yetu, kuanzia hewa ya kutufaa na maji.
Dunia ni mojawapo ya sayari zinazoelea katika anga ya ulimwengu. Kuna sayari nane zinazolizunguka jua, dunia yetu ikiwa sayari ya tatu katika mfumo wa jua na sayari zake.
Masafa baina yake na jua ni kilomita milioni 150 au kizio astronomia 1. Dunia huchukua siku 365.256 kulizunguka jua, na masaa 23.9345 kuuzunguka mhimili wake na upana wake ni kilomita 12,756.
Dunia huwa na mwezi 1.
Ni mahali pekee katika ulimwengu panapojulikana kuna uhai ulioaminiwa kuanza miaka bilioni 3.5 iliyopita[3].
Uhai unapatikana kwa spishi milioni 10-14 za viumbe hai pamoja na wanadamu waliokadiriwa kuwa sasa bilioni 7.2[4].
Umbo la dunia
Umbo la dunia linafanana na tufe au mpira unaozunguka kwenye mhimili wake. "Mhimili wa dunia" ni mstari kati ya ncha zake.
Lakini si tufe kamili. Ina uvimbe kidogo kwenye sehemu ya ikweta; ilhali umbali kati ya ncha mbili ni kilomita 12,713 lakini umbali kati ya sehemu za kinyume kwenye ikweta ni km 12,756, yaani kipenyo hiki kinazidi takriban kilomita 43 kipenyo kati ya ncha na ncha. Tofauti hii inasababishwa na mzunguko wa dunia. Kani nje inasukuma sehemu za ikweta nje zaidi. Kwa hiyo mahali duniani palipo karibu zaidi na anga la nje si Mlima Everest kwenye Himalaya bali mlima Chimborazo nchini Ekuador.[5]
Kwenye uso wake dunia huwa na tofauti kati ya nusutufe zake mbili. Nusu moja ina eneo kubwa la mabara yaani nchi kavuambayo ni asilimia 47 ya sehemu hii. Kinyume nusutufe nyingine inafunikwa na maji ya bahari na eneo la nchi kavu ni asilimia 11 pekee za maeneo yake.
Kwa jumla dunia ni sayari pekee katika mfumo wa jua yenye maji katika hali ya kiowevu usoni mwake. Bahari kuu ya dunia inashika asilimia 96.5 ya maji yote yaliyopo duniani. Maji ya bahari huwa na asilimia 3.5 chumvi ndani yake.
Kwa pamoja maeneo ya maji hufunika 70.7% za uso wa dunia. Nchi kavu huwa na 29.3% na sehemu kubwa ya eneo la nchi kavu ni bara 7 za Asia, Afrika, Amerika Kaskazini, Amerika Kusini, Antarktika, Ulaya na Australia. (Ulaya inaweza kuangaliwa pia kama sehemu ya Asia ikiwa kama rasi yake ya magharibi. Azimio la kutazama Australia kama bara na Greenland kama kisiwa tu ni azimio la hiari si la lazima).
Maeneo ya bahari kuu ya dunia kwa kawaida hugawiwa kwa bahari kubwa 3 za Pasifiki, Atlantiki na Bahari Hindi. Sehemu ya chini baharini iko kwenye Mfereji wa Mariana katika Pasifiki (mita 11,034 chini ya UB). Kwa wastani bahari huwa na kina cha mita 3,800.
Muundo wa dunia
- - taz. makala "Muundo wa dunia" -
Tumeona dunia ina umbo la mviringo au tufe. Tufe hilo si kipande kimoja kikubwa cha mwamba thabiti. Dunia ina muundo ndani yake. Muundo huo unafanana kiasi na kitunguu, yaani dunia yetu imefanyika kwa matabaka mbalimbali yanayofuatana kutoka nje kwenda ndani. Kila moja lina tabia yake.
Kimsingi wataalamu hutofautisha matabaka matatu ambayo ni:
Ganda la dunia ni sehemu imara na uhai wote tunaoujua unapatikana juu yake. Katikati hali ya koti na ya kiini ni ya joto kubwa sana na maada yake hupatikana katika hali ya giligili (si imara, kuyeyushwa). Kila ukiingia ndani dunia inazidi kuwa ya moto mpaka ukifika ndani kabisa daraja ya harara hufikia nyuzi 5000-6000 °C.
Matabaka hayo yanafanywa kwa elementi za kikemia ambazo ni feri (chuma) (32,1 %), oksijeni (30,1 %), silisi (15,1 %), magnesi (13,9 %), sulfuri (2,9 %), nikeli (1,8 %), kalsi (1,5 %) na alumini (1,4 %). Mabaki ya 1,2 % ni viwango vidogo vya elementi nyingine. Elementi hizo zinapatikana kwa hali safi au katika kampaundi za elementi.
Vipimo vimeonyesha ya kwamba matabaka mawili ya koti na kiini huwa tena na mgawanyiko ndani yake, hivyo matabaka yafuatayo yanaweza kutofautishwa.
Tabaka | Kuanzia kilomita |
---|---|
Ganda la nje | 0 - 40 |
Koti la juu | 40 - 400 |
Koti la kati | 400 - 900 |
Koti la chini | 650 - 2900 |
Kiini cha nje | 2900 - 5100 |
Kiini cha ndani | 5100-6371 |
Sehemu ya juu ya koti inafanana kikemia na ganda na sehemu hizo mbili zinaitwa tabakamwamba. Tabakamwamba ina unene wa kilomita 50 - 100.
Tabakamwamba imekatika katika vipande vinavyoitwa mabamba la gandunia. Vipande hivi vinaelea juu ya giligili ya koti la ndani. Ndiyo sababu bara lolote si la milele; kila bamba huwa na mwendo wake na ndiyo sababu katika historia ya dunia mabara yameachana na kuungana mara kadhaa. Kwa mfano imepimwa ya kwamba sehemu kubwa ya Afrika ya Mashariki ina mwendo wa kuachana na bara la Afrika na dalili yake ni bonde la ufa.
Pale ambako mabamba yanapakana, volkeno nyingi zinapatikana na matetemeko ya ardhi hutokea.
Uga sumaku wa dunia
Dunia inazungukwa na uga sumaku yaani mistari ya nguvu ya kisumaku. Sababu yake ni kwamba kiini cha dunia kinafanywa na chuma chenye tabia kama sumaku kubwa.
Tabia hiyo inasababishwa na mwendo wa mikondo ya chuma cha moto kilichoyeyuka katika kiini cha nje cha dunia. Mistari ya nguvu ya sumaku inatoka nje kwenye ncha ya kusini na kurudi ndani ya dunia kwenye ncha ya kaskazini. Tabia hiyo ni msingi wa kazi ya dira ambamo sindano ya dira huvutwa daima na ncha sumaku ya dunia na kuelekea kaskazini muda wote.
Uga sumaku wa dunia ni kinga muhimu kwa uhai wote duniani. Dunia inapigwa muda wote na mnururisho kutoka jua kwa njia ya "upepo wa jua". Mnururisho huo ni nuru pamoja miale ya hatari. Uga sumaku unakengeusha sehemu kubwa ya mnururisho hatari hadi unapita kando ya dunia na kutofika kwenye uso wa dunia.
Dunia kama mahali pa uhai
Dunia yetu ni sayari pekee inayojulikana mpaka sasa ambapo binadamu na viumbe vingine vinaweza kuishi. Hapa kuna sababu mbili
- dunia yetu ina umbali na jua unaofaa kwa maisha kwa sababu sayari zilizoko karibu zaidi na jua (k.m. Zuhura) zina joto kubwa mno na sayari zilizoko mbali zaidi kama Mrihi ni baridi mno.
- dunia yetu ina angahewa yenye asilimia 78 ya naitrojini, asilimia 21 ya oksijini na asilimia 1 ya aina nyinginezo za hewa, na kwa sababu hii uhai na maisha yanamakinika katika ardhi, kinyume na sayari nyinginezo.
Uso wa dunia
Sehemu kubwa kabisa ya dunia inafunikwa na bahari, kwani takriban asilimia 70 ya uso wake unafunikwa na maji ya bahari na kutokana na maji yote yaliyokuwepo ardhini, asilimia 97 ni maji ya bahari, na asilimia 3 ni maji matamu. Theluthi inayobaki ni nchi kavu kwenye mabara mbalimali na visiwa vingi.
Sura ya dunia ni kilomita mraba 510,066,000, ikiwa nchi kavu imechukua eneo la kilomita mraba 148,647,000 na maji yamechukua eneo la kilomita mraba 361,419,000.
Bahari Kuu | Eneo lake | Kina chake |
---|---|---|
Pasifiki | maili 64,186,000 muraba | futi 15,215 |
Atlantiki | maili 33,420,000 muraba | futi 12,881 |
Bahari Hindi | maili 28,350,000 muraba | futi 13,002 |
Bahari ya Antaktika | maili 7,848,300 muraba | futi 13,100 - 16,400 |
Bahari ya Aktika | maili 5,106,000 muraba | futi 3,953 |
Angahewa
Hewa iliyoko juu ya ardhi vile vile ina matabaka mbalimbali, na kila tabaka lina kazi yake. Hewa kwa jumla ina masafa ya kiasi cha kilomita 560 au maili 348 kuendea juu, na baada ya hapo unaingia kwenye anga la nje. Hewa hiyo ndiyo inayotukinga sisi viumbe na madhara ya jua na mnururisho wa angani ambao unaingia anga la dunia na kuteremka chini.